 |
| Mzee Gurumo akiwa na wanamuziki wenzake wa Msondo Ngoma, Hassain Moshi na Shaaban Dede |
JUZI tasnia ya muziki ilipata simanzi kubwa kutokana na maamuzi magumu
aliyoyafanya mwanamuziki gwiji nchini, Muhidin Mwalimu Gurumo 'Mjomba'
a.k.a Kamanda alipotangaza kung'atuka kwenye muziki baada ya kuutumikia
kwa miaka zaidi ya 50.
April mwaka jana (2012) nilikuwa miongoni mwa watu waliomtembea Mzee
Gurumo alipokuwa akijiuguza nyumbani na kubahatika kufanya naye
mahojiano yaliyozaa makala ndefu kuhusu alipoanzia alipotoka na
alipokuwa akielekea.
Kwa ambao hawakubahatika kuisoma makala hiyo labda wajikumbushe kidogo
historia ya mwanamuziki huyo mkongwe ambaye alikuwa tayari kugombana na
wamiliki wa bendi mradi kuwatetea wanamuziki wenzake ambao aliamini kama
siyo wao wamiliki wasingekuwa na chao na kutambulisha bendi zao.
Naiweka makala hiyo kama ilivyotoka gazeti la NIPASHE bila kupunguza
wala kuongeza neno jingine ili mradi tu wasomaji wa blogu hiii mumjue
Gurumo na kwa amewatia simanzi kwa uamuzi wake wa kujiondoa kwenye
muziki wakati bado watu wanamhitaji kuanzia wanamuziki wenzake,
mashabiki na hata taifa kwa ujumla.
=========
HUWEZI kuuzungumzia muziki wa Tanzania hasa miondoko ya dansi, bila
kulitaja jina la Muhidin Mwalimu Gurumo (sio Maalim kama baadhi
walivyozoea kumuita).
Hii ni kwa sababu mwanamuziki huyo mkongwe, maarufu kama 'Kamanda' au
'Mjomba', aliyewahi kutamba na kuziasisi bendi mbalimbali nchini
ameutumia zaidi ya nusu ya umri wake katika mambo ya muziki, hivyo kuwa
na mchango mkubwa katika fani hiyo.
Gurumo alianza fani ya muziki katika bendi za mitaani miaka ya 1950
akipitia bendi moja baada ya nyingine hadi leo akiwa na Msondo Ngoma,
ingawa ameshindwa kupanda nao jukwaani kwa siku za karibuni kutokana na
afya yake kutetereka kwa maradhi aliyonayo.
Mbali na mchango wake binafsi kama mwanamuziki, Gurumo mwenye umri wa
miaka 71 amekuwa msaada mkubwa kwa wanamuziki waliowahi kuibuliwa naye
au kufanya naye kazi kutokana na misimamo yake thabiti ya kulinda na
kutetea haki za wanamuziki.
Baadhi ya wanamuziki waliowahi kufanya naye kazi na Gurumo ni Shaaban
Dede 'Super Motisha', Bennovilla Anthony, Hassan Rehani ‘Bitchuka’ na
wengine kadhaa wakiwemo waliotangulia mbele ya haki kama Suleiman
Mbwembwe na Tx Moshi William, wamewahi kukiri jambo hilo.
"Kama viongozi wa bendi wangekuwa kama Gurumo katika kupigania na
kutetea haki za wasanii, naamini tungekuwa mbali mno, mjomba (jina
jingine la utani la Gurumo) huwa hataki mchezo," aliwahi kusema Dede.
Wakati wa mahojiano maalum na yeye yaliyofanyika hivi karibuni nyumbani
kwake Mabibo jijini Dar es Salaam, Gurumo alisema kwamba kilichokuwa
kikimsukuma kuwapigania wanamuziki wenzake na yeye mwenyewe ni dhamana
ya uongozi na hali ya umaskini aliozaliwa nao.
"Unajua mimi nimezaliwa katika familia ya kimaskini na kimekulia kwenye
umaskini, hivyo nafsi yangu huwa ngumu kumkandamiza maskini mwenzangu
kwani naamini sio haki na dhambi kubwa kwa Mungu," alisema.
"Japo nilikuwa katika nafasi ya kufanya hila kwa kuegemea upande wa
wamiliki wa bendi, ila kule kutambua kuwa uongozi niliopewa na wenzagu
umetokana na imani yao kwangu, ndio maana nilikuwa mkali kama pilipili
kuwapigania wenzangu," aliongeza.
Gurumo, alisema hata alipokuwa akishawishiwa na baadhi ya wamiliki wa
bendi ili kuwageuka wenzake ilimradi yeye aongezwe dau lolote analotaka,
hakukubali kirahisi na wakati mwingine kufikia kuamua kuhama iwapo dai
lake halisikilizwi.
"Karibu bendi zote nilizopitia misimamo yangu ilikuwa hivyo na ikitokea
uongozi ukawa mbishi kukaidi madai ninayowasilisha kwao, huwa radhi
kuondoka kama nilivyofanya OSS na kwingine," aliongeza.
Gurumo, alisema kutokana na misimamo hiyo mikali, alijikuta kila bendi
aliyojiunga nayo wanamuziki wenzake humchangua kuwa kiongozi hadi sasa
akielekea kustaafu fani hiyo kutokana na umri kumtupa mkono na maradhi
yanayomsumbua kwa hivi sasa.
Alisema, tabia yake ya kutanguliza masilahi ya wanamuziki wenzake mbele
kwa kiasi fulani yamechangia kushindwa kujijenga kimaisha kulinganisha
na umaarufu wa jina lake na umri alioutumia katika fani hiyo ya muziki.
Gurumo, alisema katika umri wa zaidi ya miaka 40 aliyotumia katika
muziki hana cha kujivunia zaidi ya kujenga nyumba yenye vyumba 17 eneo
la Mabibo, kujenga nyumba nyingine katika shamba lake lililopo kijijini
kwao Masaki, Kisarawe, mkoani Pwani.
"Nyumba hii kama unavyoiona ambayo nimewapangisha watu na ninaendelea
kuikarabati ndio pekee ya kujivunia, pia nina shamba nililojenga kibanda
kingine huko Masaki, lakini kwa hadhi yangu nilipaswa kuwa mbali na
hapa au vipi?" alisema Gurumo kwa kuhoji.
 |
| Gurumo akiwa nje ya nyumba yake ya Mabibo |
Alisema, kwa hadhi yake wala asingekuwa akipigana vikumbo na mashabiki
wake kwenye daladala aendapo kwenye shughuli zake na hata kwenye kliniki
ya matatizo yake kiafya, lakini hana jinsi kwa vile hana uwezo wa
kumiliki hata gari ndogo ya kutembelea.
"Naamini wengine wanaweza wasiamini, lakini ukweli ni kwamba sijawahi na
wala sijui ni lini nitakuwa na usafari wangu binafsi, natamani lakini
tatizo uwezo wa kifedha ndio tatizo, kama sio kujenga banda hili hapa
Mabibo, sijui ingekuwaje," alisema.
Alisema, kinachomfanya awe katika maisha hayo licha ya umaarufu wake
kimuziki, Gurumo alisema mbali na kuthamini na kujali wengine, lakini
ukweli ni kwamba enzi akiutumikia muziki hakukuwa na masilahi ya
kutosha kama wapatavyo vijana wa sasa.
"Huwa natamani miaka irudi nyuma na zama zile ziwe hivi sasa, ili nami
niweze kunufaika na jasho langu katika muziki," alisema huku tabasamu la
uchungu likimtoka usoni mwake.
MJOMBA
Mkongwe huyo aliyejifunza muziki tangu akiwa Shule ya Msingi Sungwi,
iliyopo Kisarawe akiimba na kupiga dramu katika bendi ya shule, alisema
safari yake ya muziki kwa kiasi kikubwa ilichangiwa na mjomba wake
aitwaye Seleman Sultan Wamikole.
Alisema mjomba wake aliyemchukua tangu akiwa mdogo baada ya baba yake
mzazi Mwalimu Mohammed Gurumo, kufariki na kumuacha katika maisha
magumu na ndugu zake wakiwa na mama yao Mwazani Sultan aliyefariki mwaka
1981.
Alisema kutokana na hali ilivyokuwa nyumbani kwao, mjomba wake huyo
alimchukua na kuja kuishi nae Dar es Salaam maeneo ya Ilala ambapo moja
kwa moja alimwandikisha katika madrasa ambako alipata fursa ya kuimba
kaswida.
Alisema kuwa baadaye alipata hamu ya muziki hasa kutokana na kuvutiwa na
kazi za nyota wa wakati huo, Salum Abdallah 'SAY' na Luambo Luanzo
Makiadi 'Franco'.
Alisema mjomba wake huyo akishirikiana na mama yake walitambua kiu kubwa
aliyokuwa nayo katika sanaa ya muziki na hivyo wakamruhusu kujiunga
jumla ambako alizidi kuiva na baadaye kufuatwa na bendi mbalimbali.
"Kwa kitendo nilichofanyiwa na mjomba kwa kunitunza, kunilea na
kunisaidia katika harakati zangu za muziki, ilinifanya nimtungie wimbo
maalum nilikuwa OSS miaka ya 1980, wimbo uliitwa 'Shukrani kwa
Mjomba'," alisema Gurumo.
Alisema anaamini kama sio mjomba na mama yake ambaye hadi leo anamliza
akikumbuka alivyofariki, huenda asingefikia mahala alipo sasa kimuziki.
Mtunzi na muimbaji huyo mahiri nchini, alisema licha ya kipaji cha
kuzaliwa, lakini Salum Abdallah na Franco ni watu waliochangia kufika
kwake hapo alipo kwani enzi zao walimvutia mno.
"Ni kweli kipaji cha muziki nimezaliwa nacho na kukirithi kutoka kwa
mama yangu Mwazani aliyekuwa kiongozi wa kundi la ngoma, ila kuvutiwa na
Salum Abdallah na Franco ni sababu ya mimi kufika hapa nilipo,
niliwapenda mno wanamuziki hawa," alisema.
SAFARI
Gurumo alisema baada ya kujifunza muziki kwenye makundi mbalimbali ya
mitaani, mwaka 1959 ndipo alipoanza kutambulika rasmi baada ya
kuchukuliwa na bendi ya Kilimanjaro Chacha.
Alisema alijiunga na bendi hiyo kama muimbaji ingawa pia alikuwa anamudu
kupiga dramu chombo alichokuwa akikipiga katika bendi ya shule na
ndani ya bendi hiyo ndipo alipotunga kibao chake cha kwamba kilichoitwa
'Wakati Nikiingia Bar'.
Hata hivyo Gurumo alisema hakukaa sana Kilimanjaro Chacha kwani mwaka
1962 alihama na kwenda kujiunga bendi ya Rufiji Jazz alipokutana na
wakali kama Salum Nonde, Mbarouk Khalfan na wengine.
Alisema alijiunga na bendi hiyo kutokana na kushawishiwa na safari
ambayo Rufiji Jazz ilikuwa ikitarajia kufanya mkoani Arusha na pia
maslahi, hata hivyo miezi michache baadaye aliiacha bendi hiyo na
kuhamia Kilwa Jazz B mwaka 1963.
 |
| Mzee Gurumo akiwa na baadhi ya tuzo zake wakati huo nilipomtembelea nyumbani |
"Masilahi na ujana ndiyo ulionifanya niikache bendi ile na kutua Kilwa
Jazz B, ambapo kutokana na kipaji kikubwa cha uimbaji nilichokuwa
nacho, uongozi wa Chama cha Wafanyakazi (NUTA) uliamua kunichukua na
kutua NUTA Jazz mwaka 1964," alisema.
Alisema kuwa alipotua NUTA alitunga kibao kilichokuja kumpa umaarufu cha
kilichoitwa 'Mwangele', kikiwa na maana 'Mchumba' kwa lugha ya Kingoni
na kisha kufuatiwa na nyimbo nyingine kadhaa.
"Kwa kweli idadi ya nyimbo nilizotunga nikiwa NUTA sizikumbuki kwa wingi
wake, ila baadhi ni kama "Nimuokoe Nani', 'Kaka Seleman', 'Amina',
Msondo Ngoma Na.1-4 na 'Maneno ya Nyerere'," alisema.
Gurumo alisema baada ya kuipandisha NUTA iliyokuwa ikifahamika baadaye
kwa jina la JUWATA, hasa alipowachukua wanamuziki nyota kama Bitchuka
'Stereo' na Said Mabera aliyekuwa akipuliza 'trumpet' katika bendi moja
ya Arusha, Shirika la Teksi (TTTS) lilimfuata ili kuasisi bendi yao.
"TTTS walinifuata na kunieleza nia yao ya kutaka kuanzisha bendi na
nikakubaliana nao ambapo walinilipa Sh 50,000, nikaondoka Juwata Jazz
mwaka 1978 na kuasisi bendi ya Mlimani Park 'Sikinde' nikiwa na
wanamuziki wenzangu wa Juwata na wengine kutoka Dar International,"
alisema.
Aliwataja baadhi ya waasisi wa bendi hiyo iliyokuja kufahamika kama DDC
Mlimani Park kabla ya miaka mitatu iliyopita kurejea jina lake la awali
baada ya kutemwa na mwajiri wao, Shirika la Maendeleo mkoa wa Dar es
Salaam, ni Hassani Bitchuka na marehemu Abel Baltazar aliotoka nao
Juwata.
Wengine ni Joseph Mulenga 'Spoiler', Salum Machaku, Cosmas Chidumule,
Hamis Juma 'Maalim Kinyasi', Ibrahim Mwinchande, Abdallah Gama na
George Kessy kabla ya kuongezwa nguvu na akina Michael Enoch 'Teacher',
Joseph Benard na Habib Jeff.
‘KASSIM WA KUTUMIA’
Alisema ndani ya Sikinde, kama kawaida aliendelea kutamba na utunzi wa
nyimbo zilizotwaa umaarufu mkubwa ukiwemo wa 'Kassim' uliokuwa na sehemu
mbili.
Gurumo alisema kibao hicho ni tukio la kweli lililomhusu rafiki yake
aitwaye Kassim aliyekuwa akifanya kazi katika kampuni ya mizigo uwanja
wa ndege (DAHACO), ambaye alikuwa akisifika enzi hizo kwa ulevi na
kusahau familia yake.
"Huu wimbo nilimtungia rafiki yangu ambaye alikuwa akiendekeza starehe
kupita kiasi na kila nilipokuwa nikimsihi apunguze, alikuwa akinitaka
nimuimbe ndipo ataacha ulevi," alisema.
Alisema kuwa baada ya hapo, ndipo alipoamua kutunga 'Kassim namba 1',
ambapo mwenyewe (Kassim) alikuwa akijisikia fahari, ingawa hakuacha
ulevi hadi alipopatwa matatizo kazini na kuchacha ambapo kidogo aliacha
pombe na yeye kumtungia Kassim Na.2'.
 |
| Gurumo alipokuwa amelazwa hospitali |
Gurumo alisema mpaka sasa hajui kama jamaa yake huyo aliacha pombe na
pia hajui kama yu hai au la kwa vile ni miaka mingi imepita bila kuonana
naye.
"Sijui kama yu hai au la, ila nyimbo zile zilimhusu yeye katika
kumkataza anasa ingawa pia nilikuwa natoa ujumbe kwa jamii," alisema.
Mkali huyo ambaye ni shabiki wa kutupwa wa Simba, akiwa ni mmoja wa
wanachama wake tangu mwaka 1972 na pia anayeishabikia Manchester United
ya Uingereza, alisema alikaa na Mlimani Park hadi mwaka 1985 alipojiunga
na safari Sound (OSS) akiwa na Bitchuka.
Alisema alipotua OSS aliwakuta baadhi ya wanamuziki wake ambao wengi wao
walitokea Zaire (sasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo) wakilala chini
na kuushinikiza kuwanunulia vitanda kama anataka aifanyie kazi bendi
hiyo.
Alisema kuwa kwa bahati nzuri, uongozi ulimsikiliza na kuwanunulia
wanamuziki wote vitanda kama alivyotaka na kuanza kufanya kazi ikiwemo
kubadili mtindo wa bendi hiyo wa 'Dukuduku Yee' na kuwa 'Ndekule'.
Gurumo alifichua kuwa mitindo yote aliyoasisi katika bendi za NUTA Jazz,
Mlimani Park na OSS ya 'Msondo Ngoma', 'Sikinde Ngoma ya Ukae na
'Ndekule' ni ngoma ya asili ya kabila lake la Kizaramo ambazo mama yake
alikuwa akiimba na kuzicheza enzi zake.
Alisema jambo hilo la kutumia ngoma za makabila ya kabila lake, ndilo
ambalo hata wanamuziki nyota wa nchi za Kongo na mataifa mengine ya
Afrika Magharibi wamekuwa wakifanya na kuutangaza muziki wao kimataifa
tofauti na ilivyo nchini.
 |
| Mzee Gurumo akiwa na Nyoshi El Saadat |
"Hata Wakongo na wanamuziki wa kimataifa kutoka nchi kama Senegal,
Cameroon, Nigeria na Chad wamekuwa wakibuni muziki wao kwa kutumia ngoma
za makabila yao, bahati mbaya vijana wengi wameshindwa kuumiza vichwa
nao kubuni kazi zao na kuishia kunakili kazi za wenzao bila kujua
wanawasaidia kuwatangazia, kwa kulikwepa hilo ndio maana nilikuwa
nakubuni miondoko ya kabila langu la Kizaramo," alisema.
Gurumo, alisema sio jambo baya wanamuziki wa Tanzania kuiga kazi za
wenzao, kitu alichodai ni vigumu kukikwepa, lakini alidai ni vema kama
wangekuwa wakibuni vionjo vitakavyowatofautisha na wanamuziki hao
wanaowaiga.
Alisema kwa muono wake ukiondoa Msondo na Sikinde zinazopiga muziki
unaotambulika kama dansi la Tanzania, karibu bendi zote zinapiga muziki
kwa kuwaiga wakongo, hata kwa zile bendi ambazo zilikuwa zikiaminika
kuwa ni kilelezo rahisi kuitambulisha Tanzania kimataifa.
ULEVI
Gurumo hafichi kitu juu ya ujana wake kwa kueleza mbali na 'ubitozi'
aliokuwa nao, pia alikuwa 'gangwe' enzi zake na pia aligeuzwa mtumwa wa
pombe kutokana na kuwa mlevi aliyepitiliza.
Alisema, alikuwa anakata kilaji isivyo kawaida jambo ambalo lilikuwa
likimfanya akorofishane na mama yake mzazi aliyetishia kumuachia 'laana'
kama angeendelea kuendekeza ulevi.
"Kwa wanaonijua sidhani kama hili ni jipya, nilikuwa mlevi haswaa, kiasi
mama alishindwa kunivumilia na kutishia kuniachia laana kama
nisingesikilia wito wake wa kuachana na pombe," alisema.
Alisema, baada ya kushindana na 'shetani' kwa muda mrefu akikorofishana
hata na mkewe, Pili bint Said Kitwana, hatimaye aliachana na ulevi mwaka
1982, miezi michache tangu mama yake mzazi kufariki.
"Ilikuwa ni kazi ngumu kuachana na pombe, lakini kwa heshima ya mama
niliacha, pia shinikizo la mke wangu kipenzi ambaye ninampenda na
kumsifia kwa uvumilivu wake, niliacha miezi michache baada ya mama
kufariki na hadi leo situmii hiyo kitu," alisema.
 |
| Gurumo akiwa na wanamuziki wenzake wakongwe walipokuwa wakiandaa nyimbo maalum za Tanzania All Stars |
Gurumo, alisema binafsi anajutia masuala ya ulevi akidai ni kati ya
mambo yaliyochangia kumkosesha kufanya mambo ya maendeleo pamoja na
kuihatarisha ndoa yake, kama mkewe asingekumvumilia kwa miaka 20 tangu
walipooana mwaka 1962.
"Naamini ulevi uliopitiliza kwa hakika ni mbaya kama vijana wa sasa
mnavyosema kwamba 'ulevi ni noma', nusura ndoa yangu ivunjike kwa ajili
ya kuendekeza hii kitu, hata nilipotangaza kuachana na pombe si mke
wangu wala marafiki zangu waliokuwa wakiamini hadi walipoona siku
zikienda bila kupiga kilaji," alisema Gurumo.
Gurumo alisema hakuna kitu anachofurahia maishani mwake kama siku
alipooana na mkewe, aliyezaa nae watoto wanne, Mariam aliyemzaa mwaka
1981, Mwalimu, 28, Omar na Mwazani pamoja na alipoachana na pombe.
"Hivyo ndivyo vinavyonifurahisha hadi leo, nilipomuoa mke wangu na
nilipoacha pombe, ila kwa huzuni ni kifo cha mama yangu, huwezi kuamini
hadi leo huwa nikikumbuka natokwa machozi kwa namna mama alivyokuwa
anikipenda na tulivyokuwa tunapendana na kuishi kwa upendo na furaha,"
alisema.
Gurumo, alisema maisha yake yamekuwa mikononi mwa mama yake kutokana na
baba yake kufariki mwaka 1948 wakati akiwa na miaka nane tu, ndio maana
amekuwa akimkumbuka kila mara marehemu mama yake.
BITCHUKA
Gurumo anayekula vyakula vyote halali na vyenye manufaa kwa afya yake na
kunywa juisi na soda, alisema hakuna tukio lisilofutika kichwani mwake
kama siku alipoamua kumsimamisha kazi 'swahiba' wake, Hassani Rehani
Bitchuka.
 |
| Hassain Rehani Bitchuka |
Alisema, alifanya uamuzi huo aliouita kuwa mgumu kuwahi kukutana nao
maishani kama mwanamuziki mwaka 2005, baada ya Bitchuka kugoma kushiriki
kwenye onyesho la pamoja kati ya Msondo Ngoma na African Stars 'Twanga
Pepeta'.
"Bitchuka aligoma kushiriki onyesho hilo kwa madai asingeweza kufanya
onyesho na watoto, kitu ambacho kiliwaudhi wanamuziki wenzake na wote
waliniangalia mimi kama kiongozi wao nitafanya nini kwa kosa alilofanya
'swahiba' wangu ambaye tumekuwa katika 'udugu' tangu nilipomchukua toka
Arusha mwaka 1973," alisema.
Alisema, hata hivyo alilazimika kusimama kidete kama kiongozi kwa kuweka
kando 'uswahiba' wake kwa Bitchuka, ili kuinusuru Msondo na kuitisha
kikao nilichotangaza kumtimua kundini, jambo ambalo anadai hadi leo
humpa tabu kubwa kutokana na uhusiano aliokuwa nao na Bitchuka kwa mjda
mrefu.
"Kwa kweli jinamizi la tukio lile hadi leo huniwewesesha, lakini tayari
nilishazungumza na Bitchuka na kunielewa, pia unajua wakati mwingine
ukiwa kiongozi unapaswa kufanya maamuzi magumu bila kutarajiwa,"
alisema.
Alipoulizwa juu ya msanii gani kwa sasa anayemuona kama ndiye mrithi
atakayeendeleza gurudumu la muziki wa dansi nchini, Gurumo bila kificho
alimtaja Husseni Jumbe mmiliki wa bendi ya Talent.
"Kwangu namuona Jumbe kama ndiye tumaini pekee la maendeleo ya muziki wa
dansi kutokana na kipaji kikubwa alichonacho akitunga, kuimba, kupanga
muziki na kujaliwa sauti ya kipekee," alisema.
Kuhusu muziki wa kizazi kipya, alisema upo juu kwa vile unatangazwa mno
na vyombo vya habari, ila haoni kama ni muziki wenye nguvu unaoweza
kuufunika muziki wa dansi.
"Promo ndio inayoubeba muziki huu, kitu kinachowalemaza wasanii wake
kushindwa kuwa wabunifu na kujiona wamefika mbali, wakati wana kazi
kubwa hususani ya kujifunza kupiga ala mbalimbali ili wapige muziki wao
utakaokubalika kimataifa tofauti na sasa wakitegemea kila kitu kifanywe
studio," alisema.
Hata hivyo alikiri wanaoufanya muziki huo na taarabu wamekuwa na
mafanikio makubwa kimaisha kwa vile soko limewapokea vema, jambo ambalo
hata yeye hupata wivu akifikiria anapowaona vijana wakiendesha magari
wakati yeye akitembea kwa miguu licha ya muda mrefu aliotumia kwenye
fani hiyo ya muziki.
SWAHIBA WA JK
Gurumo, alisema fani yake ya muziki imemsaidia kufahamiana na wengi
wakiwemo viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi, huku akimtaja Rais
Jakaya Kikwete kwamba ni mmoja wa viongozi 'rafiki' zake.
Alisema, urafiki huo ndio anaoamini ulimfanya Rais Kikwete kuvunja
shughuli zake na kumtembelea hospitalini kumjulia hali alipolazwa kwa
mara ya kwanza kutokana na maradhi yanayomsumbua.
Gurumo, alisema kitendo cha Rais Kikwete kuacha kazi zake kwendsa
kumjulia hali na kumsaidia katika matibabu yake kumemfariji mno, kwa
vile katika kulazwa kwake na hata sasa akiendelea kujiuguza nyumbani
hakuna kiongozi yeyote wa serikali wakiwemo wa Wizara wa Habari na
Utamaduni, kuwahi kwenda kumjulia hali.
 |
| Rais Kikwete akimtunukia tuzo Mzee Gurumo wakati wa uzinduzi wa TBC |
"Huwezi amini ni yeye na mkewe, Mama Salma ndio waliokuja kunijulia hali
hospitalini, akianza mwenyewe kisha mkewe kitu ambacho kinanifariji
hadi leo nikiamini Rais Kikwete anatujali na kututhamini wasanii,"
alisema.
Aliongeza kuwa, ukiondoa kufarijika kwake kutembelewa hospitalini na
Rais Kikwete na mkewe, Mama Salma, pia kitendo kilichofanya na
Mkurugenzi wa ASET, Asha Baraka cha kuandaa onyesho maalum kwa ajili ya
kumchangia ni kitu ambacho kitabaki kichwani mwake na kumpongeza
mwanamama huyo maaraufu kama 'Iron Lady'.
"Kwa kweli sikutarajia kama Asha Baraka angeweza kufanya kitendo kile
ambacho ni wazi ninaonyesha ni jinsi gani anavyothamini na kujali
mchango katika muziki. Nadhani watu wengine wanapaswa kuiga mfano wake,
ni mtu ambaye ameonyesha mapenzi kwangu na kujali mchango wangu katika
muziki, namshukuru na kumpongeza," alisema.
Gurumo, anayechizishwa na rangi nyekundu na nyeupe na ambaye anapenda
kutumia muda wake za ziada kujishughulisha na mambo ya Kilimo kwenye
shamba lake lililopo Masaki, alisema katika maisha yake kisanii amewahi
kupata tuzo mbili tu zote za mwaka 2008.
Alisema tuzo hizo ni ile ya Kili Music Award kama Mwanamuiki Mkongwe na
ile ya Hall of Fame, huku aliyekuwa mdau mkubwa wa muziki nchini
aliyekuwa akifanya shughuli zake Umangani, Is'haka Kibene alimtengenezea
na kumpa tuzo maalum kumtambua kama 'Kamanda wa Muziki wa Tanzania.
 |
| Mzee Gurumo
akipokea msaada wa fedha toka kwa Asha Baraka 'Lady Iron' anayetajwa na
gwiji huyo kama mwanamke wa mfano Tanzania katika kuuthamini mchango
wake kisanii Tanzania |
UBUNIFU
Gurumo, aliyeanza kuonekana tena kwenye jukwaa la bendi yake ya Msondo
baada ya kuwa nje kwa wiki kadhaa kutokana na kulazwa hospitalini,
alisema muziki wa Tanzania umepiga hatua kubwa kimaendeleo, ingawa
alikiri kwamba kukosekana kwa ubunifu miongoni mwa wananamuziki na
wasanii wake ni tatizo linaloukwaza usitambe nje.
Alisema, hata muziki wa kizazi kipya (bongofleva) ambao umekuwa ukitajwa
kama wenye maendeleo makubwa kwa wasanii wake, alisema unashindwa
kutamba kimataifa kwa sababu wasanii hao hawaumizi vichwa kubuni vitu
vipya.
Mkongwe huyo alisema tatizo la wasanii kupenda kuiga kazi za wenzao wa
nje na kuzifanya zao kwa kuziimba kiswahili, ndilo linalowafanya
wasitambe kimataifa na kutaka kuwepo kwa mabadiliko kuanzia sasa.
Alisema suala la kuiga kazi za nje halijaanza sasa, bali kitamboi kirefu
akikiri hata wao (wakongwe) walikuwa wakifanya hivyo, ila alisema
ubunifu wa ziada ndio uliowafanya waonekane mahiri katika soko la
kimataifa.
"Kuiga ni jambo lisilokwepeka, lakini ni wajibu wa wasanii wa sasa
kuumiza vichwa na kubuni vitu vipya ambavyo vitawatofautisha na
wanaowaiga. Sio Bongofleva wala dansi kote wamelemaa kwa kuiga kazi za
wenzao," alisema.
Alisema cha ajabu hata bendi za zamani ukiondoa Msondo Ngoma na Mlimani
Park, zote hushindana kupiga muziki wa kikongo bila kujua wanasaidia
kuutangaza muziki wa nchi hiyo na kuzidumaza bendi zao tofauti na Msondo
na Sikinde.
Aliongeza anahisi bendi hizo zimeamua kuingia kwenye mkumbo huo kutokana
na upepo wa soko ulivyo, japo alisema kimezifanya bendi husika
zisiwasisimue mashabiki wake kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
KUSTAAFU
Gurumo, alisema hana muda mrefu kabla ya kutangaza kustaafu fani ya
muziki kutokana na hali yake ya kiafya na umri mkubwa alionao akitaka
kuwapisha wanamuziki wenye damnu changa kuendelea gurudumu la fani hiyo.
 |
| Mzee Gurumo alipotangaza kung'atuka kwenye muziki kando yake ni Meneja wa Msondo, Said Kiberiti na Juma Mbizo |
Alisema, ingawa hajajua ni lini atafanya hivyo ila hadhani kama
utamalizika mwaka huu wa 2012 kabla ya kutimiza azma hiyo na kudai
atakapostaafu atajikita kwenye kuwasaidia vijana chipukizi.
Gurumo, alisema mipango yake ni kuanzisha chuo cha muziki anachotaka
kukijenga Masaki, Kisarawe iwapo atapata mtu wa kumsaidia kufanikisha
hilo kwa lengo la kutaka kuendeleza vipaji na kuudumisha muziki wa
Tanzania.
"Sina muda mrefu kabla ya kustaafu rasmi muziki, sitajiweka kando kabisa
na ndoto zangu ni kutaka kujenga chuo cha muziki katika shamba langu
lililopo Masaki, lakini natatizwa na hali ya kiuchumi, hivyo kama
serikali au mtu yeyote mwenye uwezo kifedha akinisaidia nitafurahi kwa
vile nataka kuendeleza muziki wetu," alisema.
Alisema, anaamini vijana wanapaswa kujifunza mengi kutoka kwake na kwa
wakongwe wengine ili kuufanya muziki wa Tanzania uendelea kudumu hasa
katika kipindi hiki cha mabadiliko ya kidunia.
FAMILIA
Muhidini Mwalimu Gurumo, alizaliwa mnamo mwaka 1940 katika kijiji cha
Masaki, Kisarawe akiwa ni mtoto wa pili kati ya watatu wa mzee Mwalimu
Mohammed Gurumo.
Baba yake alifariki wakati Gurumo akiwa na miaka nane tu na hivyo maisha
yake ya utotoni kuwa chini ya mama yake mzazi kabla ya kuchukuliwa na
mjomba wake aliyemsaidia kuingia kwennye muziki.
Gurumo, alifanikiwa kufunga ndoa na mkewe, Pili bint Said Kitwana na
kubahatika kuzaa nae watoto wanne, ambapo ni mmoja tu aitwae Mariam
ndiye aliyerithi kipaji chake cha muziki akiimba kundi moja la taarabu
lililopo Temeke.
Mkongwe huyo anayemtaja Said Mabera 'Dokta' kama mmoja wa wanamuziki
viongozi anayemzimia, alisema katika maisha yake ya ndoa hakuna
anachokifurahia kama kudumu kwa ndoa yake na mkewe ambayo imetimiza
miaka 50 mwaka huu.
Alisema, kama sio uvumilivu wa mkewe, huenda ndoa hiyo ingevunjika
kitambo kutokana na ukweli ukiondoa ulevi na kazi yake ya sanaa, pia
ukorofi aliokuwa nao uliochangiwa na ujana ni kati ya mambo yaliyotaka
kuivunja ndoa yake.
"Sio siri najivunia kuwa na mke mvumilivu kama huyu, kuna mambo
niliyomfanyia kwa muda mrefu ndani ya ndoa yetu, lakini alinivumilia
hadi leo tukiingia mwaka wa 50 tangu tuoane mwaka 1962," alisema.
Aliongeza, kuwa anaamini ndoa yao ilikuwa mipango ya Mungu ndio maana
wamedumu na kuzeeka pamoja wakiwa ndio kwanza wanapendana kama wameoana
jana, jambo ambalo linamfanya kila mara kumshukuru Mungu.
MKEWE
Pili Bint Said Kitwana, alikiri kwamba ndani ya uhusiano wa kimapenzi
hadi kuja kuoana na Gurumo alipitia katika misukosuko mingi, lakini
anashukuru Mungu alijaliwa uvumilivu na kuidumisha hadi leo.
Mama huyo alisema ugomvi wake mkubwa na mumewe ilikuwa ni tabia yake ya
ulevi, hali iliyomfanya mara kwa mara kukwaruzana nae akimsihi aache.
 |
| Mzee Gurumo akiwa na mkewe, Pili bint Said |
Alisema, kuna wakati mumewe alikuwa akiondoka nyumbani Ijumaa kwenda
kwenye maonyesho na asionekane hadi Jumatatu akiletwa na rafiki zake
akiwa 'bwii', kitu kilichokuwa kikimuuma.
"Tatizo kubwa baina yangu na Gurumo ilikuwa suala la ulevi, hata alipokuja kuacha sikuamini," alisema.
Aliongeza, jingine ni tabia ya kuwa na 'kuchakachua nje', na kumfanya
aumie roho hasa wanawake zake wa nje kumfuata na kumtukana na hata
wakati mwingine kutaka kupigana nao hasa anapoamua kuambatana nae kwenye
maonyesho.
Alisema, ukiondoa matatizo hayo, Gurumo ni mume bora, mpole, mkarimu na
baba anayejali familia mwenye mapenzi ya dhati, ndio maana aliamua
kumvumilia hadi leo na kutoa wito kwa wanandoa wengine kuvumiliana
katika ndoa zao ili kuzifanya zidumu kama ilivyo kwao.
Pia, alisema kitu kinachomfurahisha kwa Gurumo ni tabia ya kutochagua
chakula cha kula, akidai hula chakula chochote isipokuwa 'kitimoto'.
Mama huyo alisema kwa namna mumewe alivyojitolea ndani ya taifa hili
kupitia fani yake ya muziki ni vema serikali ikamkumbuka kwa kumsaidia
angali akiwa hai, badala ya kusubiri aje afe ndipo wajitokeze kumwagia
sifa lukuki.
"Naiomba serikali imsaidie mzee huyu, huwa naumia roho tunapokuwa
tukipelekana klinini jinsi abiria ndani ya daladala wanavyotushangaa,
najua ni kutokana na jina kubwa la Gurumo na hali aliyonayo kimaisha,"
alisema.
Aliongeza, ingelikuwa ni amri yake angependa kuona Gurumo akipumzika
masuala ya muziki baada ya kuutumikia kwa zaidi ya miaka 50.
Mwisho
NB:Inawezekana Mzee Gurumo aliuzingatia
ushauri huo wa mkewe na kuamua kupumzika muziki majuzi akitarajiwa
kuagwa rasmi kwa matamasha ili kumchangia fedha za 'pensheni' yake
katika muziki. MICHARAZO inamtakia kila la heri mkongwe huyo na Allah SW
ampe siha, afya na umri mrefu zaidi Inshallah.