Release No. 123
  TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
  Novemba 25, 2011
  FAINALI UHAI CUP YASOGEZWA
Mechi  ya fainali ya michuano ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 ya Kombe  la Uhai (Uhai Cup) kwa klabu za Ligi Kuu sasa itachezwa kesho (Novemba  26 mwaka huu) saa 3.00 asubuhi kwenye Uwanja wa Karume.
Awali  fainali hiyo kati ya Simba ambayo iliingia hatua hiyo kwa kuitandika  Toto Africans mabao 4-1 na Azam iliyofuzu kwa kuizamisha Serengeti Boys  (timu ya Taifa ya vijana chini ya miaka 17) mabao 3-0 ilikuwa ichezwe  leo (Novemba 25 mwaka huu) saa 9.00 kwenye uwanja huo.
Mabadiliko  hayo yamefanyika ili kutoa nafasi kwa mashabiki kushuhudia mechi za  michuano ya Kombe la Chalenji inayoanza leo (Novemba 25 mwaka huu)  kwenye Uwanja wa Taifa. Kila siku kwenye michuano ya Chalenji zinachezwa  mechi mbili; ya kwanza saa 8.00 mchana na nyingine saa 10.00 jioni.
Michuano  ya Kombe la Uhai inadhaminiwa na Kampuni ya S.S. Bakhresa kupitia maji  Uhai ambapo bingwa atapata sh. milioni 1.5, mshindi wa pili sh. milioni  moja wakati wa tatu atapata sh. 500,000. Mbali ya fedha hizo, bingwa  atapata medali za dhahabu, makamu bingwa medali za fedha na mshindi wa  tatu medali za shaba.
Mchezaji bora sh. 400,000, mfungaji bora (sh. 300,000), kipa bora (sh. 300,000) na timu yenye nidhamu sh. 300,000.
VIINGILIO MICHUANO YA KOMBE LA CHALENJI
Viingilio  kwa mechi za hatua ya makundi kwa michuano ya Kombe la Chalenji  inayoanza leo (Novemba 25 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam vitakuwa kama ifuatavyo;
Kwa  viti vya rangi ya bluu na kijani ambavyo ni zaidi ya 30,000 kiingilio  kitakuwa sh. 1,000 wakati viti vya rangi ya chungwa ambavyo ni zaidi ya  10,000 kiingilio kitakuwa sh. 3,000. VIP C na B ambayo jumla ya viti  vyake ni 8,000 kiingilio kitakuwa sh. 5,000 wakati VIP A yenye viti 700  kiingilio ni sh. 10,000.
Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
No comments :
Post a Comment