
Francis Boniface Cheka 'Maputo'
Na Imani Makongoro, Mwananchi
Nyumbani kwa
 bondia Francis ‘SMG’ Cheka hakuishi pilika ambazo zinatokana na kazi ya
 chupa za plastiki anayofanya bingwa huyo wa zamani wa dunia wa WBF.
Nje ya 
nyumba yake kuna mafurushi kila kona yakiwa na ‘bidhaa’ tofauti ikiwamo 
chupa za plastiki, chupa za konyagi, chibuku na plastiki ngumu (ndoo na 
madumu) yaliyopasuka.
Cheka anavyookota chupa
“Mimi ndiyo 
mwanzilishi wa biashara hii hapa Morogoro, niliianza 2004 baada ya 
kuamua kuingia mtaani kuokota na kuziuza mwenyewe, wakati huo kilo moja 
niliuza kwa Sh100 na nilikuwa nikizunguka kutwa nzima kutafuta chupa 
mtaani,” anasema Cheka.
Anasema wakati anaanza kuokota chupa alikuwa na miaka mitano tangu aingie kwenye ngumi za kulipwa, lakini hakuwa maarufu.
“Nilikuwa 
nina uwezo wa kuzunguka na kuokota hadi kilo 100 kwa siku, japo ilikuwa 
kazi ngumu, lakini nilipata fedha nikanunua kiwanja maeneo ya Kilimahewa
 na kujenga nyumba kwa kazi ya kuokota chupa.
“Pia 
niliweza kujiandalia mapambano peke yangu kwa kazi hii, ambayo 
yalinijenga na kunipa umaarufu kwenye ngumi, nimejiandalia mapambano 
zaidi ya 15 kwa fedha niliyopata kwa kuokota chupa,” anasema Cheka.
Anasema 
vijana wengi wa Morogoro walianza kuokota chupa baada ya kuona Cheka 
amejenga nyumba kwa kazi hiyo, hivyo hakuwa na hiyana aliwafundisha kazi
 hiyo na wengine aliingia nao mtaani kuokota.
“Nilipoanza 
kucheza mapambano ya ubingwa wa Afrika nilisimama kuokota chupa 
nikawaachia wengine na mimi kuelekeza nguvu zangu kwenye ngumi, kijiwe 
changu nikamweka mtu wa kufanya hiyo kazi na nikawa na nanunua kwa watu 
wengine kisha mimi nauza tena.
“Kwa kipindi
 chote ambacho nilikuwa nimebanwa na masuala ya ngumi, mradi wangu huu 
uliyumba kwani kila niliyemwachia alikuwa na fikra za kuniibia, ilifikia
 mahali nikakwama kwani nilikopa fedha benki kuongezea nguvu kwenye 
biashara yangu ya makopo hivyo nilipaswa kulipa,” anasema Cheka.
Anavyookota chupa mtaani
“Watu 
wanashangaa mtu kama mimi kuokota chupa, lakini ndiyo kazi inayoniweka 
mjini, wiki iliyopita nilikuwa Msamvu (stendi kuu ya Morogoro) nakusanya
 chupa kwa bahati nikakutana na Naibu Waziri wa Habari, Vijana, 
Utamaduni na Michezo, Juma Nkamia alishangaa kuniona naokota Chupa.
“Hakuamini 
kama mimi bingwa wa dunia na bondia namba moja Tanzania ndiyo naokota 
chupa mtaani, lakini ukweli nisipofanya kazi hii na nikabaki kutegemea 
ngumi, maisha yatakuwa magumu kwangu,” anasema Cheka.
Anasema 
haoni aibu kufanya kazi hiyo kwani ni kazi iliyompa mafanikio na kujenga
 nyumba mbili, moja ikiwa Kilimahewa ambako anaishi hivi sasa na 
nyingine Kihonda alikowapangisha watu wengine.
“Muda wangu 
mwingi nimeelekeza kwenye chupa, mazoezi sasa sifanyi kwani nina muda 
sijafanya mazoezi ya ngumi, nasimamia mwenyewe biashara yangu ya chupa 
ambayo mbali na kuokota mwenyewe pia kuna watu ambao wanaokota na 
kuniuzia.
“Chupa za 
maji nanunua kilo moja Sh250 na mimi nauza 700 baada ya kusaga, kwa 
mwezi nina uhakika wa kuuza kilo 4,500 mpaka 6,000 na plastiki ngumu 
nanunua Sh350 na mimi nauza Sh 2,000 baada ya kusaga hivyo kwa mwezi 
nauza zaidi ya kilo 3,000, pia naokota chupa za konyagi na chibuku 
ambazo naziosha na kuwauzia watu wa kampuni hizo,” anasema Cheka.
Ameamua kuingia mtaani kutembeza CD
“Sijapata 
mafanikio yoyote kwenye ngumi hadi sasa hivyo nimeona nijaribu kuuza CD 
za mapambano yangu labda nitafanikiwa,” anasema Cheka.
Anasema kazi
 hiyo anaifanya kwa kutembeza CD zake mkononi na kuwapelekea watu kwenye
 maeneo tofauti mjini Morogoro na amekwishauza CD 200 hadi sasa.
“Nilitoa CD 
200 ambazo niliziuza kwa kutembeza mwenyewe mkononi zikaisha na sasa 
nimetoa nyingine 200, najitangazia biashara mwenyewe kwani napeleka 
kwenye mkusanyiko wa watu, vituo vya daladala, Stendi ya Msamvu na 
maeneo ambayo najua nikienda sikosi wateja, CD moja nauza Sh 3000,” 
anasema Cheka.
Fedha nyingi aliyowahi kupata katika ngumi
“Fedha 
nyingi niliyopata ni Sh10 milioni ambayo nilicheza pambano Russia mwezi 
Desemba 2012 na kupigwa kwa Knock Out (KO) raundi ya nne, pambano lile 
nilicheza bila kujiandaa na nilipata fedha hiyo kwa kuwa sikuitumia 
kwenye maandalizi,” anasema Cheka.
Anasema 
mapambano mengi anayocheza nchini amekuwa akiambulia Sh3 milioni mpaka 
Sh4 milioni baada ya kutoa fedha za maandalizi, kumlipa kocha na kununua
 vifaa.
“Pambano 
nililocheza na Mmarekani la ubingwa wa dunia nilipewa Sh4 milioni za 
maandalizi, nikaweka kambi Nairobi kila kitu nalipa mwenyewe mpaka 
kumlipa kocha, hadi narudi sina fedha baada ya pambano nikapewa Sh3 
milioni, nilikuwa na madeni nikalipa na kubaki sina kitu.
“Hata wakati
 nafanyiwa sherehe ya kupongezwa Morogoro, sikuwa na hata shilingi, siku
 nawekewa dau la Sh10 milioni nikacheze Russia, sikukataa japo nilijua 
sina mazoezi, nilipigwa KO kihalali na kuvuliwa ubingwa wa dunia,” 
anasema Cheka.
Mkakati wake wa kurudi shule
Cheka 
alipewa ofa ya masomo kwenye Chuo cha St Joseph cha mjini Morogoro na 
aliingia darasani siku moja kisha akatokomea hadi leo hajawahi kurudi.
“Mimi ni 
baba wa familia ambayo inanitegemea, siyo kama sipendi kusoma, lakini 
nikiwa shule majukumu ya familia nitayatekeleza vipi? Hivi sasa nimeamua
 habari ya kusoma niiweke kando niboreshe biashara yangu, Mungu 
akiniweka hai, nitasoma miaka ijayo,” anasema Cheka.
Kwa nini anaitwa Kazimoyo?
Akiwa Morogoro, Cheka anajulikana pia kwa jina la Kazimoyo.
“Hili jina 
nimepewa na marafiki zangu ambao wananiita Kazimoyo kutokana na kazi 
ninazozifanya, ambazo wanasema nina moyo mgumu ndiyo sababu nazifanya, 
hivyo kazi ninazofanya sasa na nilizowahi kufanya nimefanya kwa moyo 
tu,” anasema Cheka.
Historia fupi ya maisha yake
Cheka 
alizaliwa miaka 32 iliyopita jijini Dar es Salaam, akiwa mtoto wa kwanza
 kwa baba yake, Boniface Cheka na alisoma Shule ya Msingi Kinondoni 
Hananasifu.
Alianza kucheza ngumi akiwa darasa la tatu na wakati huo baba yake alipenda kumfundisha ngumi.
“Nilipohitimu
 shule ya msingi, nilipata kazi kwenye gari la taka la Manispaa ya 
Kinondoni, nilifanya kazi hiyo pia nikijifua ngumi kwenye Ukumbi wa 
Arnautoglu, Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.
“Baada ya 
kuona maisha magumu Dar es Salaam, Nilikwenda Morogoro, sikuwa na mahali
 pa kufikia hivyo nikaomba kazi ya kufagia Stendi ya Msamvu na usiku 
hapo ndipo nikawa nalala,” anasema Cheka.
Anasema 
alilazimika kutandika maboksi na kulala kituoni hapo usiku ulipoingia na
 asubuhi anaamkia kwenye kibarua cha kufagia kituo hicho.
“Nilipata 
fedha kidogo na kupanga chumba, nakumbuka kitanda changu nilinunua kwa 
fedha niliyopata kwenye kazi ya kuzibua choo, sikuwa na ujuzi huo, 
lakini rafiki zangu waliponiambia kuna kazi hiyo nilienda kufanya na 
kulipwa Sh50,000 ambayo ilikuwa fedha nyingi kuwahi kulipwa,” anasema 
Cheka.
Anasema 
baada ya muda ndipo aliingia mtaani kuokota chupa, kazi iliyompa 
mafanikio na kujenga nyumba, na kutumia fedha aliyopata kujitangaza 
kwenye ngumi.
CREDIT: MWANANCHI
No comments :
Post a Comment