CHAMA cha
 Wananchi (CUF) kimesema hakiikubali Katiba inayopendekezwa kwa kuwa 
haina maslahi ya wananchi wa Zanzibar.
Badala yake chama hicho kimewataka
 Wazanzibari waikatae Katiba iliyopendekezwa na Bunge Maalum la Katiba 
(BMK).
Kauli 
hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu wa CUF ambaye pia ni Makamu wa Kwanza
 wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad, wakati akihutubia 
mkutano mkubwa wa hadhara katika viwanja vya Demokrasia vya Kibanda 
Maiti, mjini Zanzibar.
“Wananchi,
 Katiba haikubaliki kwa Wazanzibari, mimi mwenzenu siikubali, sijui 
nyinyi wenzangu?” alihoji Maalim Seif na wananchi kuitikia kuwa nao 
hawaikubali.
Alisema 
kuwa miongoni mwa mambo yanayoipokonya Zanzibar hadhi yake ni Katiba 
inayopendekezwa kumpokonya Rais wa Zanzibar mamlaka ya kugawa mikoa, 
tofauti na Katiba ya Zanzibar ya sasa. 
Alisema
 kwa maana hiyo Rais wa Muungano anachukua mamlaka ya Rais wa Zanzibar 
na anaweza kuteuliwa wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya wa Zanzibar. 
“Kwa
 mabadiliko hayo ya rasimu ya Chenge, Rais wa Muungano anaweza 
kututeulia Sheha wa Shehia ya Mtoni Zanzibar kutoka Bukoba,” alisema 
Maalim Seif huku akishangiliwa na wanachama na wafuasi wa CUF.
Maalim
 Seif alisema Katiba ya Zanzibar na marekebisho yake ya mwaka 2010 iko 
sahihi kabisa na inazingatia matakwa ya Makubaliano ya Muungano.
Alisema hayuko tayari kuona rasimu hiyo inakubalika na kwamba Wazanzibari hawataki kuiona.
Alisema
 hakubaliani na kauli za baadhi ya watu waliosema kuwa Serikali ya 
Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) inaridhishwa na mchakato wa Katiba mpya.
“Nataka
 kuwambia hakuna kikao chochote cha SMZ kilichokaa na kusema tunaijadili
 rasimu, kama kuna mtu anataka kusema eti Smz imeridhishwa aseme 
mwenyewe binafsi na siyo Serikali ya Umoja wa Kitaifa,” alisema Maalim 
Seif.
Maalim
 Seif aliisifu Rasimu ya Jaji Joseph Warioba ambayo ndiyo ilizingatia 
matakwa ya Watanzania walio wengi na kwamba pamoja na awali Wazanzibari 
kupendekeza muundo wa Muungano wa mkataba, lakini kwa busara ya tume 
hiyo waliikubali muundo wa serikali tatu.
Maalim
 Seif alisema anahutubia mkutano huo akiwa na furaha kubwa kutokana na 
umma ulioteremka katika viwanja vya Kibandamaiti, na hiyo ni sababu 
tosha na ujumbe kuwa hawaitaki Katiba inayopendekezwa.
“Ndugu 
yangu, rafiki yangu Rais Jakaya Kikwete ufahamu kuwa umma huu 
uliohudhuria Kibandamaiti ni ujumbe tosha kuwa Katiba hiyo hawaitaki, na
 mwambia Rais Kikwete kuwa Katiba hii hatuikubali,” alisema Maalim 
Seif. 
Maalim 
Seif alisema Katiba bora ni ile inayozingatia maoni ya wananchi. 
“Lakini
 Rais (Rais Jakaya Kikwete), Katiba yenu mmeweka upande maoni ya 
wananchi, mmejifungia wenyewe, mmeipitisha wenyewe na mmeichezea ngoma 
wenyewe”, alisema. 
Naibu 
Katibu Mkuu wa CUF, Nassor Ahmed Mazrui, alisema wajumbe saba wa Bunge 
Maalum la Katiba waliopiga kura ya Hapana hadharani kukataa rasimu hiyo 
ni mashujaa wa Zanzibar na Wazanzibari wote wanapaswa kuwapa heshima 
kubwa.
Mkurugenzi
 wa Habari na Uenezi wa CUF, Salum Bimani, alisema wananchi wa Zanzibar 
wameshaamua na hawatarejea nyuma zaidi ya kuiondoa CCM mwaka 2015 na 
kuipa Zanzibar mamlaka kamili.
Bimani alisema msiwape kura viongozi wa CCM ambao wanauza nchi ya Zanzibar huku wakicheza ngoma.
“Kwa
 Shilingi 300,000 watu hawa wanadiriki kuuza nchi, hawa waliopiga kura 
za ndiyo ni madalali wa Zanzibar, hata wale waliopiga kura za siri pia 
ni madalali,” alisema Bimani.
Alisema wanasheria wawili wameitetea Zanzibar na wakafikwa na masahiba mazito.
Aliwataka wanasheria hao kuwa Jaji Walfgong Dourado na Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliyefutwa kazi, Masoud Othman Masoud.
Bimani
 alisema Wazanzibari wapo pamoja nao katika kuhakikisha Zanzibar inabaki
 na wale wenye nia mbaya wajue kwamba Zanzibar wataitapika watake 
wasitake. 
Mansour alisema naendelea kuwa muumini wa Maridhiano ya Zanzibar. Katiba hii ni yao wenyewe si ya Wazanzibari.
“Baada ya kuona umma huu uliohudhuria katika mkutano huu tunapaswa kumhofia Mwenyezi Mungu,” alisema.
“Naendelea
 kumuunga mkono Maalim Seif Sharif Hamad, ni kiongozi asiyekuwa mnafiki 
anajitambua na hatawaliwi na utawala wa Dodoma, anatawaliwa na 
Wazanzibari wenyewe na matakwa na matumaini yao,” alisema na kuwataka 
Wazanzibari wasiwe na hofu kwani hawawezi kufungwa wote wako wengi sana,
 wakati umefika. 
“Tumeungana
 kwa hiari yetu, tukakubali kwa hiari yetu, sisi si watumwa wa mtu 
yoyote, tumefungwa tumefukuzwa makazini kwa sababu ya nchi hii, hatuwezi
 kurudi nyuma,” alisema.
Alieleza
 kuwa watu wasishangae kumuona Mwenyekiti wa Kamati ya Maridhiano, Mzee 
Nassoro Moyo, amesimama kwenye jukwa anatetea nchi yake.
Mzee Moyo alisema Wazanzibari hawakubalini kuona watu wanataka kuichukua nchi yao ovyo ovyo.
Mkutano
 huo ambao ni wa kwanza kuhutubia na Maalim Seif tangu BMK limalize kazi
 yake na kuwasilisha rasimu kwa Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar,
 Dk. Ali Mohammed Shein, ulihudhuriwa na maelefu ya wananchi huku baadhi
 yao wakibeba mabango.
Baadhi
 ya mabango hayo yalibeba ujumbe usemao “Wapige mabomu rasimu yao 
hatuitaki, Hongera Othman Masoud, Katiba ya vijisenti (Chenge) 
hatuitaki”. 
Katika 
hatua nyingine, Maalim Seif alikanusha taarifa kwenye mitandao kuwa 
hatajiuzulu wadhifa huo na ataendelea kukiongoza CUF kushika madaraka na
 kushika Serikali ya Umoja wa Kitaifa katika uchaguzi mkuu wa mwakani, 
akiwa kwenye nafasi hiyo.
Maalim
 alisema taarifa zilizoenezwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa baada ya 
kufukuzwa Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar, Masoud Othman Masoud, naye 
amejiuzulu Umakamu wa Kwanza ni uzushi mtupu.
CHANZO: NIPASHE
No comments :
Post a Comment