BAADA ya kulileta nchini Kombe la Ligi Kuu ya Uingereza, benki ya Barclays Tanzania huenda ikadhamini Ligi Kuu ya soka Tanzania bara baada ya Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuifungulia milango benki hiyo kufanya nayo mazungumzo.
Akizungumza na Waandishi wa habari Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Rished Bade juu ya ujio wa kombe hilo, alisema hiyo ni mara ya kwanza kwa kombe hilo kutua hapa nchini kitendo ambacho kitazidi kuongeza mashabiki wa ligi hiyo hapa nchini.
Amesema kombe hilo litakaa nchini kwa siku mbili kuanzia jana na leo ambapo litazungushwa katika mitaa mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam ambapo wamefanya hivyo ili kutoa nafasi kwa wadau wa michezo kuliona kombe hilo.
''Benki ya Barclays imeongeza mkataba wa kuendelea kudhamini ligi ya Uingereza mpaka mwisho wa msimu wa ligi wa mwaka 2012/13 ambapo kwa kipindi hicho Barclays itadhamini kwa paundi za Uingereza milioni 82.25,'' alisema Bade.
Akijibu baadhi ya maswali juu ya kombe hilo kutua nchini na Watanzania watafaidika vipi nalo, alijibu kuliona tu itakuwa faraja kubwa na pia kwa sasa wapo katika mazungumzo na BMT na TFF juu ya kudhamini ligi kuu ya Tanzania bara.
Amesema mazungumzo hayo yanaendelea na wana imani yatafikia pazuri kwani dalili za mvua ni mawingu, hivyo wadau wa soka wanatakiwa wawe wavumilivu juu ya suala hilo.
Ameongeza watashirikiana na Mwenyekiti wa BMT, Idd Kipingu katika kuhakikisha kuanzia mwakani wanaandaa programu ya kupeleka vijana wadogo katika vituo vya Michezo huko Uingereza ili Tanzania nayo iwe na wachezaji wengi wa kulipwa.
Naye Kipingu alisema, wamejisikia faraja kuona mwaka huu makombe yote makubwa Duniani na maarufu yanakuja hapa nchini, hivyo ni fursa pekee kwa wachezaji wa Tanzania kuzidisha juhudi ili tusiwe wageni wa makombe hayo.
Amesema anaishukuru Barclays kwa kulileta kombe hilo nchini kwani katika ya matazamaji milioni 500 duniani, Watanzania nao wapo wengi hivyo sasa watajionea wenyewe pia hata wanapozishangilia baadhi ya timu za huko waweze kufarijika.
Pia aliongeza kwamba wanaiomba Barclays itie nguvu katika kudhamini mashindano ya vijana na yale ya wanawake ili waondokane na kila siku kuwa wasindikizaji katika mashindano ya Kimataifa.
No comments :
Post a Comment