
Na Tiganya Vincent-MAELEZO-Dar es salaam
 SERIKALI ya Japan imepatia Tanzania msaada wa shilingi bilioni 
28.2 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mitatu ya uboreshaji wa usafiri 
jijini Dar es salaam na kilimo hapa nchini.
 Msaada huo umesainiwa (leo)
 jijini Dar es salaam na Balozi wa Japan hapa nchini Masaki Okada kwa 
niaba ya Japan na Waziri wa Fedha Dkt. William Mgimwa kwa niaba ya 
Serikali ya Tanzania.
 
Akizungumza mara baada ya kusaini msaada huo Waziri wa Fedha Dkt . 
Mgimwa alisema kuwa mradi wa kwanza utahusisha upanuzi wa barabara ya 
Kilwa na ile ya Bandari ambapo jumla ya shilingi bilioni 20 zitatumika 
katika kukamilisha mradi huo.
 
Aliongeza kuwa mradi mwingine ni ule wa ujenzi wa barabara za 
juu(flyover) katika makutano ya TAZARA ambapo jumla ya shilingi bilioni 
moja (1) na milioni 26 zinatarajiwa kutumika katika kukamilisha mradi 
huo.
 
Dkt. Mgimwa aliongeza kuwa eneo lingine ambalo litanufaika na msaada 
kutoka Japan ni kuunga mkono sera ya Kilimo kwanza ambapo Tanzania 
imepata shilingi bilioni sita(6) na milioni 92 kwa ajili ya kuhakikisha 
kunakuwepo kwa usalama wa chakula cha kutosha katika maeneo mbalimbali 
hapa nchini.
 
Alisema kuwa upande wa eneo hilo lengo ni kuhakikisha kuwa Watanzania 
wengi wa kipato cha chini wanaboresha kilimo ambacho kitawahakikisha 
uhakika wa chakula wakati wote na hivyo kuondokana na umaskini.
 
Kwa upande wa Balozi wa Japan hapa nchini Masaki Okada alisema kuwa 
wananchi wengi wa Tanzania hasa wakazi wa Jiji la Dar es salaam wamekuwa
 wakisubiri kwa hamu barabara za juu ili kusaidia kupunguza msongamano 
wakati wa kuja na kutoka katikati ya jiji la Dar es salaam.
 
Alisema kuwa utakapo kamilika mradi huo utasaidia kupunguza tatizo la 
msongamano na hivyo kupunguza saa za mwananchi kusafiri kuja na kutoka 
katikati ya jiji la Dar es salaam.
 
Balozi Okada alisema kuwa hatua hii itakuwa muhimu katika kukuza uchumi 
kwani wananchi watakuwa na muda wa kutosha kuzalisha mali kutoka na 
miundombinu kuruhusu magari kwenda kasi pasipo kikwazo.
No comments :
Post a Comment